Misri: Rais Abdel Fattah al-Sisi kuwania kwa muhula wa tatu
Nairobi – Rais wa Misri Abdel Fattah al-Sisi amethibitisha kuwa atawania awamu ya tatu katika uchaguzi mkuu uliopangwa kufanyika mwezi Desemba.
Imechapishwa:
Kiongozi huyo wa zamani wa jeshi amekuwa madarakani tangu kuangushwa kwa utawala wa Mohammed Morsi mwaka wa 2013.
Wanaharakati kwenye taifa hilo wanasema kwamba chini ya uongozi wa rais Abdel Fattah, wanasiasa wa upinzani wamekuwa wakikandamizwa, uchumi wa taifa hilo pia ukizorota.
Katiba ya taifa hilo ilifanyiwa marekebisho miaka mine iliyopita kuongeza muda wa rais kusalia madarkani.
Wapinzani wamekuwa wakiituhumu utawala wake kwa kuzuia majaribio yao ya kutaka kuwania urais.
Uchaguzi huo, ambao El-Sisi anatazamiwa kwa kiasi kikubwa kushinda, unakuja wakati huu Misri ikikabiliana na mzozo wa kiuchumi, mfumuko wa bei, sarafu ya ndani iliyopungua na madai ya upinzani kwamba wagombea wake wananyanyaswa na kukabiliwa vitisho.
Takriban raia milioni 65 nchini humo wanatarajiwa kupiga kura katika uchaguzi huo, ambao utafanyika kwa siku tatu kuanzia Desemba 10 hadi 12.
Raia wa taifa hilo wanaoishi nchi ya nchi wataweza kupiga kura kati ya Disemba 1-3.
El-Sisi alitangazwa mshindi wa uchaguzi wa urais mwaka 2014 na 2018 kwa asilimia 97 ya kura.