Guinea: Doumbouya ataka mataifa ya Afrika kuheshimiwa
Nairobi – Kiongozi wa kijeshi nchini Guinea, Kanali Mamady Doumbouya, katika hotuba yake kwenye mkutano Mkuu wa Umoja wa Mataifa, ametetea uamuzi wa jeshi katika nchi za Afrika, kuchukua madaraka, akitaka mataifa ya Magharibi kuacha kuingilia masuala ya Afrika.
Imechapishwa:
Doumbouya alichukua madaraka kupitia mapinduzi ya kijeshi mwezi Septemba mwaka 2021, baada ya miaka 11 ya utawala wa kiraia nchini Guinea.
Aidha ameeleza kuwa mfumo wa kidemokrasia wa mataifa ya Magharibi haufanyi kazi katika mataifa ya bara Afrika.
"Sisi Waafrika tumechoka namna ya hawa na wale mnavyotupangia, hatuungi mkono na hatupingi Marekani, hatuungi mkono na hatuwapinga Wachina, hatuungi mkono wala hatiwapingi Wafaransa, hatuungi mkono wala hatuwapingi Warusi, sisi ni Waafrika tu." alisema kanali Mamady Doumbouya.
Kanali Mamady Doumbouya
Kanali Mamady amesema jeshi nchini mwake liliamua kuchukua madaraka kwa sababu hatua hiyo ndiyo ilikuwa ya kipekee kuepusha taifa hilo kuingia katika machafuko.
Raia jijini Conakry walionekana kushangilia hatua hiyo ya mapinduzi yaliongusha utawala wa rais Conde.
Jumuiya ya Ecowas ilisitisha uanachama wa taifa hilo kutoka katika muungano huo baada ya mapinduzi hayo na kutaka kurejeshwa kwa utawala wa kiraia.
Mwaka jana kanali Doumbouya hakutoa ratiba ya muda wa kipindi cha mpito na kurejeshwa kwa utawala wa kidemokrasia baada ya mazungumzo na Ecowas japokuwa hakuna hatua zilizopigwa kupanga uchaguzi.
Guinea ni miongoni mwa mataifa ya Afrika Magharibi na ya kati kukabiliwa na mapinduzi ya kijeshi ikiwemo Mali, Burkina Faso, Niger na Gabon.
Mapinduzi hayo yamekashifiwa na Ecowas, Umoja wa Afrika na Umoja wa Mataifa.