Somalia: EU imesitisha kwa muda utoaji wa misaada kutokana na madai ya ufujaji
Nairobi – Umoja wa Ulaya umethibitisha kusitisha kwa muda malipo kwa shirika la mpango wa chakula duniani WFP kwa ajili ya kutoa misaada ya kibinadamu nchini Somalia.
Imechapishwa:
Msemaji wa tume ya Umoja wa Ulaya, Balazs Ujvari, amesema hatua hiyo imechukuliwa kama njia moja ya kulinda fedha za Umoja huo.
Uchunguzi uliofanywa na Umoja wa Mataifa ulibaini kuwepo kwa wizi wa misaada inayotolewa nchini Somalia kwa ajili na maofisa katika taifa hilo, maofisa wa usalama ambapo pia wafanyikazi wa misaada wanahusishwa na sakata hilo.
Mwaka jana Umoja ya Ulaya ulitumia zaidi ya Dolla milioni saba sawa na pauni milioni 5.6 kwa ajili ya kuendeleza shughuli za shirika la mpango wa chakula duniani WFP nchini Somalia.
Kwa upande wake shirika la misaada la nchini Marekani limesema halina mpango wa kusitisha msaada wa utoaji wa chakula kwa Somalia.
Mamilioni ya watu nchini Somalia wanahitaji chakula cha msaada kutokana na ukame wa muda mrefu katika pembe ya Afrika pamoja na utovu wa usalama unaosababishwa na wapiganaji wa Al shabab, hali ambayo imesababisha idadi kubwa ya raia kwenda kuishi katika kambi za wakimbizi.