Rais Ali Bongo anazuiliwa nyumbani kwake: Jeshi
Nairobi – Wanajeshi nchini Gabon wanasema rais Ali Bongo Ondimba anazuiliwa nyumbani kwake wakati huu pia mmoja wa wanawe wa kiume akizuiliwa kwa tuhumu za uhaini.
Imechapishwa:
Mwanawe Bongo wa karibu zaidi Noureddin Bongo Valentin, mkuu wake wa wafanyakazi Ian Ghislain Ngoulou pamoja na naibu mshauri wake, washauri wengine wawili wa rais na maafisa wakuu wawili wa chama tawala cha Gabon Demokratik (PDG) wamekamatwa kwa mujibu wa kiongozi wa jeshi.
Wanatuhumiwa kwa uhaini, rushwa na kughushi saini ya rais, miongoni mwa tuhuma nyinginezo.
Mapema Jumatano, maofisa wa kijeshi walisema wameupindua utawala wa Bongo, ambaye amekuwa madarakani kwa miaka 14, saa chache baada ya kutangazwa mshindi katika uchaguzi wa Jumamosi.
Katika taarifa ya televisheni, walisema matokeo ya kura yamefutwa na "taasisi zote za jamhuri" zilivunjwa.
Bongo ambaye amekuwa madarakani kwa miaka 14, alikuwa ameshinda uchaguzi kwa awamu ya tatu kwa kupata asilimia 64.27 ya kura.
Mpîzani mkuu wa Bongo, Albert Ondo Ossa, alipata asilimia 30.77 ya kura hizo kwa mujibu wa matokeo.
Tayari China imetoa wito kwa pande zote nchini Gabon kutoa usalama kwa rais Ali Bongo, wito unaokuja baada ya kundi la wanajeshi kudai kumaliza utawala wa sasa kwenye taifa hilo.
Msemaji wa wizara ya mambo ya nje ya China Wang Wenbin ameeleza kuwa nchi yake pia inafuatilia kwa ukaribu hali inayoendelea nchini Gabon.
Beijing inapendekeza kufanyika kwa mazungumzo ya pande zote nchini humo kwa manufaa ya raia na kurejeshwa kwa hali ya kawaida haraka iwezekanavyo.