Gabon: Yajiandaa kwa ajili ya uchaguzi, rais Bongo asaka muhula wa tatu
Nairobi – Wananchi wa Gabon, siku ya Jumamosi, watapiga kura kumchagua rais, wabunge na wawakilishi wa manispaa.
Imechapishwa:
Tume ya uchaguzi, imewasajili wapiga kura 850,000 wanaotarajiwa kushiriki kwenye uchaguzi huo katika taifa hilo la Afrika ya Kati lenye watu zaidi ya Milioni 2.3.
Rais Ali Bongo, ambaye amekuwa madarakani tangu mwaka 2009, baada ya kifo cha baba yake Omar Bongo, aliyeongoza kwa miaka 42 tangu 1967.
Bongo anatafuta muhula mwingine wa miaka saba, baada ya mwaka 2016 alipata ushindi mwembamba kwa kumshinda mpinzani wake Jean Ping kwa kura 5,500.
Familia ya Bongo, imeongoza Gabon kwa miaka 55 na inaripotiwa kuwa tajiri, unaotokana na uwepo wa mafuta nchini humo.
Kuelekea uchaguzi huu, Bongo amekuwa akisumbuliwa na changamoto ya kiafya baada ya kupata kiharusi Oktoba mwaka 2018, na kutoonekana kwa muda miezi 10.
Mwezi Januari mwaka 2019, alikabiliwa na jaribio la jeshi kutaka kumwondoa madarakani.
Anawania kwa muhula wa tatu, akikabiliwa na upinzani mkali kutoka kwa Albert Ondo Ossa, anayeungwa mkono na vyama sita vya upinzani.
Kuna wagombea wengine 12, lakini hawana umaarufu. Wachambuzi wa siasa wanatabiri kuwa rais Bongo, atatangazwa mshindi kwenye uchaguzi huo.