Ujumbe wa Ecowas wazuru Niger, kuzungumza na uongozi wa kijeshi
Nairobi – Ujumbe wa ECOWAS umewasili nchini Niger kwa mazungumzo na wanajeshi waliotekeleza mapinduzi kwa mujibu wa ripoti kutoka kwa watu wa karibu na jumuiya hiyo na rais aliyeondolewa madarakani Mohamed Bazoum.
Imechapishwa: Imehaririwa:
Ziara hii inakuja wakati huu Jumuiya hiyo ikiwa imekubali kuweka tayari kikosi chake kinachotarajiwa kutumika nchini Niger iwapo suluhu la kidiplomasia halitapatikana.
Jumuiya hiyo inasema licha ya kuweka tayari kikosi chake kumrejesha madarakani rais Bazoum, inaweka mbele juhudi za mazungumzo.
Ujumbe huo umewasili jijini Niamey siku moja baada wakuu wa kijeshi katika Jumuiya hiyo kusema kwamba wako tayari kuingilia kati kumrejesha madarakani rais Bazoum.
Utawala wa kijeshi nchini Niger umethibitisha kuwasili kwa ujumbe wa Ecowas kwenye taifa hilo ukiongozwa na kiongozi wa zamani wa Nigeria Abdulsalami Abubakar.
Awali ujumbe wa ECOWAS ukiongozwa na Abubakar ulijaribu kukutana na viongozi wa kijeshi nchini Niger mapema mwezi huu bila ya mafanikio ya kukutana na jenerali Abdourahamane Tiani.
Viongozi wa ECOWAS wanasema lazima wakabiliana na kinachoendelea nchini Niger ambalo ni taifa la nne Afrika Magharibi kukabiliwa na mapinduzi ya kijeshi tangu mwaka wa 2020 baada ya Mali, Guinea na Burkina Faso.