Wakuu wa kijeshi wa Ecowas wanakutana kujadili hali ya Niger
Nairobi – Wakuu wa kijeshi kutoka nchi za Afrika Magharibi, Ecowas, wanakutana kujadili mpango wa kuweka tayari kikosi cha jeshi kwa ajili ya kuingilia kati urejeshaji wa utawala wa kidemokrasia nchini Niger.
Imechapishwa:
Viongozi hao wanakutana jijini Acra nchini Ghana kwa muda wa siku mbili kuaanzia leo Alhamis hadi kesho Ijuma.
Karibia wanachama 11 kutoka katika jumuiya hiyo yenye wanachama 15 wanaunga mkono hatua ya matumizi ya nguvu za kijeshi kumrejesha madarakani rais Mohamed Bazoum, baada ya njia za kidiplomasia kuonekana kutozaa matunda.
Mkutano huo unafanyika wakati huu mataifa matatu wanachama wa Ecowas yakiwa ni Mali, Burkina Faso na Guinea yakiwa chini ya uongozi wa kijeshi.
Tayari viongozi wa mapinduzi ya huko Niger wameonya kujibu na kujilinda iwapo njia zozote za kijeshi zitatumika kuingilia kati kinachoendelea nchini mwao.
Kikao hicho kinachofanyika jijini Accra kinatarajiwa kujadili kuhusu ufadhili, idadi ya wanajeshi na kanuni za oparesheni za maofisa wa kijeshi wa Ecowas huko Niamey.
Mkutano huu unafanyika wakati huu hali ya kiusalama ikionekana kuendelea kuwa mbaya huko Niger.
Siku ya Jumanne, wanajeshi 17 waliuawa wakati wengine 20 wakijeruhiwa katika shambulio la watu wenye silaha.