Niger itashinda vikwazo vya Ecowas: Waziri mkuu
Waziri mkuu mpya wa Niger Ali Mahaman Lamine Zeine, katika mahojiano yaliochapishwa leo Jumatatu amesema nchi yake itashinda vikwazo vilivyotangazwa dhidi yake na Jumuiya ya Ecowas.
Imechapishwa:
Kiongozi huyo ameiambia DW kwamba licha ya kuwa sio sawa kutangaziwa vikwazo hivyo, kama taifa wataweza kushinda.
Jumuiya ya Ecowas ambayo imetangaza vikwazo dhidi ya Niger kufuatia mapinduzi ya kijeshi nchini humo awali ilikuwa imetishia kutumia nguvu za kijeshi kumrejesha madarakani rais Mohamed Bazoum aliyechaguliwa kwa njia ya kidemokrasia kabla ya kuondoa mpango huo.
Ecowas imetangaza vikwazo vya kifedha, kukata usambazaji wa umeme pamoja na kufunga mipaka yake na Niger ambayo haina bandari hali ambayo imezuia usambazaji wa bidhaa kwenye taifa hilo masikini duniani.
Awali jeshi lilikuwa limesema vikwazo hivyo limefanya kuwa vigumu kwa raia nchini humo kupata bidhaa muhimu kama vile dawa, chakula na umeme, jeshi likitaja hatua hiyo kama kinyume na sheria na isiyokuwa yakujali masilahi ya binadamu.
Zeine aidha ameelezea matumaini kuhusu ziara ya ujumbe kutoka Nigeria na mazungumzo na Ecowas ambapo pia amesisitiza umuhimu wa kuwepo kwa uhusiano mwema kati ya Niger na Nigeria pamoja na mataifa mengine ya Ecowas.