Niger: EU inasema haitowatambua wanajeshi waliohusika na mapinduzi
Umoja wa Ulaya umesema hautowatambua wanajeshi wa Niger waliohusika na mapinduzi na kwamba unasitisha makubaliano ya kiusalama na taifa hilo linalokabiliwa na ukosefu wa usalama unaoendelezwa na makundi ya kijihadi.
Imechapishwa:
Abdourahamane Tchiani, jenerali ambaye ameongoza kitengo cha ulinzi wa rais tangu mwaka wa 2011, alijitangaza kuwa kiongozi mpya wa taifa hilo la Afrika Magharibi siku ya Ijumaa kupitia televisheni ya kitaifa.
Walinzi wa rais walimzuia kiongozi aliyechaguliwa kwa njia ya kidemokrasia Mohamed Bazoum na kumshikilia katika makazi yake kwenye jiji kuu la Niamey siku ya Jumatano ya wiki hii.
Mataifa jirani kama vile Mali na Burkina Faso nayo pia yameshuhudia mapinduzi ya kijeshi tangu mwaka wa 2020, nchi hizo za ukanda wa Sahel zikikabiliwa na changamoto la kiusalama kutoka kwa wanajihadi wanaohusishwa na wapiganaji wa Islamic State na Al-Qaeda.
Mkuu wa sera za kigeni katika umoja wa ulaya Josep Borrell, amesema EU haitawatambua viongozi wa kijeshi waliotekeleza mapinduzi.
Aidha EU imesema ushirikiano wote katika nyanja ya usalama umesimamishwa kwa muda usiojulikana pamoja na bajeti ya misaada.
Bazoum "anasalia kuwa rais pekee halali wa Niger", taarifa hiyo ilisema, ikitaka aachiliwe mara moja na kuwataka viongozi wa mapinduzi kuwajibika kwa usalama wake na familia yake.
Borrell alisema EU iko tayari kuunga mkono maamuzi yatakayochukuliwa na jumuiya ya kikanda ya Afrika Magharibi, "ikiwa ni pamoja na kutangazwa kwa vikwazo".