MSF inataka kurejelewa kwa mpango utoaji wa misaada nchini Ethiopia
Nairobi – Madaktari wasio na mipaka (MSF) wametoa wito wa kurejelewa kwa haraka mpango wa utoaji wa chakula cha msaada nchini Ethiopia wakionya kwamba hatua ya kusitisha mpango huo imekuja wakati huu ambapo kunaripotiwa visa vingi ya utapia mlo.
Imechapishwa:
Shirika la mpango wa chakula duniani WFP na USAID yalisitisha utoaji wa misaada kwa taifa hilo la pili kwa ukubwa zaidi barani Afrika mwezi Juni kwa misingi kwamba misaada hiyo ilikuwa haiwafikii walengwa.
Kwa mujibu wa MSF, zaidi ya watu milioni 20 nchini Ethiopia walikuwa wanategemea kwa sehemu kubwa chakula hicho cha msaada, shirika hilo likionya kwamba visa vya utapia mlo vilikuwa juu hata kabla ya kusitishwa kwa mpango huo.
Wiki hii, shirika la misaada katika umoja wa mataifa OCHA liliripoti kuongezeka kwa sehemu kubwa ya utapia mlo katika eneo la Tigray nchini Ethiopia ambapo mapigano ya miaka miwili kati ya serikali ya shirikisho na wapiganji wa TPLF yalimalizika mwezi Novemba mwaka jana.
Serikali ya Ethiopia ilikashifu hatua hiyo ya kusitisha usambazaji wa chakula na kuahidi kufanya uchunguzi wa pamoja na shirika la USAID, kubaini madai kwamba chakula hicho kilikuwa kinapelekwa kwengine.