Somalia: Serikali kuchukua kambi zilizokuwa zinakaliwa na wanajeshi wa AU
Nairobi – Vikosi vya usalama nchini Somalia vimechukua majukumu ya kiusalama katika maeneo sita ambapo wanajeshi wa umoja wa Afrika walikuwa wakilinda usalama.
Imechapishwa:
Wizara ya ulinzi ya Somalia katika taarifa yake imeshukuru juhudi zilizofanywa na vikosi hivyo vya AU pamoja na nchi zilizowatuma wanajeshi wake nchini humo zikiwemo Burundi, Djibouti, Ethiopia, Kenya na Uganda.
Taarifa ya Mogadishu ikija baada ya sehemu ya wanajeshi wa AU waliokuwa wakilinda usalama nchini Somalia wakitarajiwa kuwa wameondoka kufikia tarehe 30 ya mwezi Juni mwaka huu.
Baadhi ya kambi zilizokuwa zinatumika na wanajeshi hao wa AU ikiwemo ile ya maofisa wa Burundi tayari zimekabidhiwa kwa jeshi la serikali ya Somalia.
Wanajeshi wengine elfu tatu wa umoja huo wanatarajiwa kuondoka nchini humo kufikia mwisho wa mwezi Septemba kabla ya vikosi vyote kutakiwa kuwa vimeondoka kufikia mwishoni mwa 2024.
Umoja wa Afrika umekuwa ikiisaidia serikali ya Somalia kukabiliana na wapiganaji wa al-Shabab tangu mwaka wa 2007.