Sudan: Makabiliano mapya kati ya jeshi na wapiganaji wa RSF yaripotiwa
Nairobi – Mapigano makali kati ya Jeshi la Sudan na wanamgambo wa RSF yameendelea kushuhudiwa jijini Khartoum, wakati huu kukiwa na wasiwasi wa kuzuka kwa magonjwa kama utapiamlo miongoni mwa watu waliokimbia makaazi yao.
Imechapishwa:
Cheza - 00:58
Makabiliano yalianza kushuhudiwa Jumapili asubuhi Kaskazini mwa jiji la Khartoum, baada ya wanamgambo wa RSF kujaribu kushambulia maeneo yanayodhibitiwa na wanajesjhi wa Sudan.
Milio ya risasi na mashambulio ya angaa yalishuhudiwa pia Mashariki mwa jiji hilo kuu, huku wanamgambo wa RSF wakidai kuangusha ndege ya jeshi katika eneo la Bahri, Kaskazini mwa Khartoum.
Licha ya kuwepo kwa shinikizo za kikanda na Kimataifa, hakuna dalili za kumalizika kwa vita hivi, vilivyoanza Aprili 15.
Mpaka sasa watu zaidi ya Elfu tatu wameuawa kutokana na vita hivi, kwa mujibu wa Tume ya Umoja wa Mataifa inayoshughulikia wakimbizi, huku wengine Milioni 2 nukta 2 wakiyakimbia makaazi yao, wakiwemo zaidi la Laki sita waliopewa hifadhi katika mataifa jirani.
Umoja wa Mataifa na mashirika ya kimataifa ya kutoa misaada, yanasema watu Milioni 25 wanahitaji misaada ya haraka ya kibinadamu nchini Sudan.