Sudan: Mashambulio ya angani yameshuhudiwa mazungumzo yakiendelea mjini Jeddah
NAIROBI – Wakati huu mazungumzo yanayolenga kusitishwa kwa mapigano nchini Sudan yakiendelea nchini Saudi Arabia, mashambulio ya angani yamesikika katika mji wa Khartoum mapema leo Jumamosi makabiliano yakiingia katika wiki yake ya pili sasa.
Imechapishwa:
Mmoja wa walioshuhudia mapigano hayo katika mji wa Magharibi mwa Khartoum ameeleza kuwa wanajeshi wa Sudan wamekabiliana na wapiganaji wa RSF wakati huu raia wakiendelea kukabiliwa na changamoto za kupata huduma muhimu.
Zaidi ya watu 750 wameuawa maelfu ya wengine wakiripotiwa kuyahama makazi yao tangu mapigano kati ya makundi mawili ya kijeshi yalipoaanza tarehe 15 ya mwezi Aprili.
Watu Zaidi ya milioni moja wameripotiwa kutoroka katika mji wa Khartoum peke tangu kuaanza mapigano hayo kwa mujibu wa ripoti ya umoja wa mataifa.
Raia katika mji huo wa Khartoum wanakabiliwa na changamoto za kupata matibabu baada ya hosipitali kuporwa wakati wa makabiliano kati ya wanajeshi wa wapiganaji wa RSF.
Kando na uhaba wa dawa, raia katika mji huo pia wanakabiliwa na ukosefu wa chakula na umeme, ikihofiwa kuwa huenda idadi ya wanaokabiliwa na ugumu huo ikaongezeka iwapo mapigano hayo yataendelea.
Wawakilishi wa pande mbili zinazopigana nchini Sudan wanakutana katika mji wa Jeddah nchini Saudi Arabia kwa wiki moja sasa, mazungumzo yanayolenga kusitisha mkabiliano nchini humo.
Haya yanajiri wakati huu Sudan ikitoa wito kwa jamii ya kimataifa ikiwemo umoja wa mataifa, umoja wa Afrika na mashirika mengine ya kikanda kutoa msaada wa kibindamu kwa raia wa taifa hilo .
Katibu mkuu wa umoja wa mataifa Antonio Guterres ameeleza matumaini yake kwamba mazungumzo yanayofanyika mjini Jeddah yataleta suluhu ilikuwasaidia walioathirika na mapigano yanayoendelea.