Sudan: Mapigano mazito yameripotiwa licha ya muafaka wa kusitishwa kwa saa 72
NAIROBI – Makabiliano mazito yaliohusisha ndege za kivita na mabomu yameripotiwa jijini Khartoum nchini Sudan wakati huu mapigano kati ya makundi mawili ya kijeshi yakiingia wiki yake ya tatu licha ya kuwepo kwa makubaliano ya kusitishwa kwa vita.
Imechapishwa: Imehaririwa:
Sudan imeendelea kukabiliwa na machafuko tangu mapigano kuaanza tarehe 15 ya mwezi Aprili kati ya wanajeshi watiifu kwa mkuu wa vikosi vya serikali jenerali Abdel Fattah al-Burhan na wale wa naibu wake Hamdan Daglo, anayeoongoza kikosi cha Rapid Support Forces (RSF).
Burhan na Daglo wamekuwa wakitangaza kukubaliana kusitishwa kwa mapigano tangu kuaanza kwa vita hivyo japokuwa hakuna maafikiano yanyoonekana kuheshimiwa.Kila upande ukituhumu upande mwengine kwa kuvunja mkataba wa makubaliano.
Makubaliano ya hivi punde ya kusitishwa vita kwa muda wa siku tatu yaliaafikiwa siku ya Alhamis baada ya mazungumzo yalioongozwa na Marekani, Saudi Arabia, Umoja wa Afrika na Umoja wa Ulaya yakiwa na nia ya kuafikia suluhu la kudumu.
Baadhi ya raia wa Sudan wameripoti na kuthibitisha kuwepo kwa makabiliano katika baadhi ya miji nje na jiji la Khartoum.
Raia milioni tano wa Khartoum wamesalia katika nyumba zao, ukosefu wa maji na chakula ukiwa ni mojawapo ya changamoto zinazowakabili raia hao.
Makundi mawili yatuhumiana
Wakati mapigano yakiendelea, waku wa vikosi viwili vinavyopigana wameendelea kutuhumiana katika vyombo vya habari, jenerali Burhan akiwaita wapiganji wa RSF kama magaidi wanaolenga kuharibu Sudan, kupitia mahojiano aliyofanya na runinga ya Alhurra yenye makao yake nchini Marekani.
Aidha Burhan ameeleza kuwa mamluki wanaingia nchini Sudan wakitumia mpaka wa Chad, Jamhuri ya Afrika ya kati na Niger wakiwa na nia ya kujinufaisha na mzozo huo.
Katika mahojiano na BBC, Daglo alimtaja mkuu wa jeshi nchini Sudan kama mtu asiyeaaminika na msaliti.
Watu 512 wamethibitishwa kuawaua katika mapigano hayo, wengine 4,193 wakiwa wamejeruhiwa kwa mujibu wa takwimu za wizara ya afya nchini humu, idadi hiyo ikihofiwa kuwa huenda ikapanda. Karibia raia 75,000 wametoroka nchini Sudan.
Maelfu ya raia wengine wameripotiwa kukimbilia katika mataifa jirani ya Chad, Misiri, Ethiopia na Sudan Kusini, mataifa ya kigeni yakiwa yamewaondoa raia wake katika taifa hilo.
Uingereza imesema itakamilisha zoezi la kuwaondoa raia wake walio nchini Sudan kufikia leo Jumamosi baada ya kuwasafirisha raia wake 1,500 na familia zao wiki hii.
Umoja wa mataifa hapo jana Ijumaa ulisema kuwa wafanyikazi wake wa kimataifa waliokuwa wamesalia nchini Sudan walikuwa wameondolewa mjini Darfur.
Shirika la mpango wa chakula duniani katika umoja wa mataifa WFP limeonya kuwepo kwa uwezekano wa mamilioni ya raia wa Sudan kukabiliwa na baa la njaa kutokana na mapigano yanyoendelea.
Tayari inakadiriwa kuwa raia milioni 15 wa Sudan wanahitaji msaada.