Sudan: Pande hasimu zakubaliana kuongeza muda wa usitishaji mapigano tena
NAIROBI – Jeshi la Sudan na wanamgambo wa Rapid Support Forces, wamekubaliana kuongeza muda wa kusitishwa kwa mapigano, lakini makabiliano yameripotiwa jijini Khartoum na Magharibi mwa jimbo la Darfur.
Imechapishwa: Imehaririwa:
Mkataba wa saa 72 wa kusitisha vita ulimalizika saa sita Alhamisi usiku, pande zote mbili zinazopigana zimekubali kuongeza mkataba mwingine wa saa 72 baada ya Marekani na Saudi Arabia kuongoza mazungumzo mengine.
Hata hivyo, ripoti zaidi zinasema mataifa kama Norway, Uingereza na Falme za Kiarabu zimeshinikiza pia kuongezwa kwa muda zaidi ili kutafuta mwanya wa mazungumzo kati ya pande hizo mbili, huku muungano wa nchi za Afrika Mashariki IGAD ukiendelea na jitihada za kukutanisha pande zote kwa ajili ya mazungumzo jijini Juba.
Licha ya makubaliano hayo, milio ya risasi na milipuko mizito imesika Kaskazini mwa jiji la Khartoum na huko Darfur na kuendelea kuzua wasiwasi miongoni mwa raia, wakati huu maelfu ya watu wakiendelea kukimbia jiji kuu, wakiwemo raia wa kigeni.
Mapigano hayo ya wiki mbili sasa kati ya jeshi la serikali na kundi hasimu la kijeshi yamesababisha vifo vya mamia ya raia, maelfu ya wengine wakilazimika kutoroka nchini humo.
Kwa mujibu wa waziri wa mambo ya kigeni wa Marekani Antony Blinken ambaye nchi yake imekuwa mstari wa mbele kutoa wito wa kusitishwa kwa mapigano na kufanyika kwa mazungumzo, amesema wanafanya kazi kubwa kuhakikisha kunakuwepo na mkataba wa usitishaji mapigano.