Sudan: Mapigano yameripotiwa licha ya ahadi ya kusitisha makabiliano
NAIROBI – Milio ya risasi imendelea kusikika nchini Sudan licha ya kuwepo kwa makubalinao ya kusitisha mapigano kuanzia usiku wa kuamkia leo.
Imechapishwa:
Mapigano yameripotiwa katika maeneo ambayo yanazunguka makao makuu ya jeshi na uwanja wa ndege ambao umezungukwa na makazi ya watu.
Majenerali wawili wapinzani ambao wamekuwa chanzo kikuu katika mzozo wa mapigano hayo walikuwa wamekubali kusitishwa kwa mzozo huo usiku wa kuamkia leo.
Kumeripotiwa hali ya dharura huku wakazi wakikosa chakula hali inayohofiwa kuwa huenda ikawa mbaya zaidi iwapo makabiliano hayatasitishwa.
Mapigano pia yamekuwa yakifanyika kwingineko nchini Sudan, ikiwa ni pamoja na Darfur upande wa magharibi.
Mkuu wa misaada ya Umoja wa Mataifa ameonya kuhusu ripoti zinazosema wafanyakazi wa misaada ya kibinadamu wanashambuliwa na kudhalilishwa kingono.
Takriban watu 200 wameuawa katika mapigano hayo yaliyoanza siku ya Jumamosi. Shirika la Msalaba Mwekundu na Shirika la Afya Duniani WHO yakiendelea kutoa wito wa kuruhusu usafirishaji wa misaada ya kibinadamu.
Haya yanajiri wakati huu Japan ikiwa inapanga kutuma ndege ya kijeshi kuwaondoa raia wake nchini Sudan wakati huu taifa hilo linapokabiliwa na mapigano kati ya pande mbili za kijeshi.
Msemaji wa serikali ya Japan Hirokazu Matsuno alisema kufikia Jumatano, kulikuwa na raia 60 wa Japani waliokwama nchini Sudan.