Zaidi ya watu 190 wamejeruhiwa katika machafuko nchini Sudan
NAIROBI – Balozi wa Umoja wa Ulaya nchini Sudan, Aidan O'Hara, ameshambuliwa nyumbani kwake mjini Khartoum, ambako mapigano makali yameendelea kushuhudiwa kati ya vikosi vinavyohasimiana. Hayo yanawadia wakati ambapo hospitali zikishambuliwa kwa makombora kwa siku ya tatu hali ambayo imesababisha vifo vya watu takriban 200.
Imechapishwa:
Wagonjwa katika mji mkuu, Khartoum, wameomba kurejeshwa kwa usalama huku mapigano ya bunduki yakiendelea katika mji huo.
Kwa mujibu wa muungano wa madaktari nchini humo, ghasia kati ya jeshi na kundi la wanajeshi maalum la Rapid Support Forces RSF zimesababisha vifo vya takriban watu 200.
Muungano wa Wafanyakazi wa Madaktari nchini Sudan unasema kwamba kumekuwa na uharibifu mkubwa katika hospitali ya mafunzo ya al-Shab mjini Khartoum, pamoja na hospitali zingine mbili, uliosababishwa na mapigano na kurushiana makombora.
Katika hatua nyingine Balozi wa Umoja wa Ulaya nchini Sudan, Aidan O'Hara, ameshambuliwa nyumbani kwake mjini Khartoum lakini hakujeruhiwa, waziri wa mambo ya nje wa Ireland Micheál Martin amethibitisha.
Martin alielezea shambulio hilo kama ukiukaji mkubwa wa majukumu ya kuwalinda wanadiplomasia.
Jeshi na kundi la RSF linadai kudhibiti maeneo muhimu mjini Khartoum, ambapo wakaazi wamekuwa wakijikinga na milipuko.
Wakati huo huo Waziri wa Mambo ya Nje wa Marekani Antony Blinken amefanya mazungumzo na majenerali wawili wanaoongoza vikosi vinavyopigana nchini Sudan na kusisitiza dharura ya kusitisha mapigano.
Blinken alisisitiza wajibu wa majenerali hao wawili kuhakikisha usalama na ustawi wa raia, wafanyakazi wa kidiplomasia, na wafanyakazi wanaotoa misaada ya kibinadamu.