Sudan: RSF inasema imesitisha mapigano kwa saa 24
NAIROBI – Kitengo cha wanajeshi maalum nchini Sudan Rapid Support Forces (RSF) kimesema kinasitisha mapigano kwa muda was saa 24 zijazo ikiwa ni njia moja ya kutoa nafasi kwa raia kupata misaada ya kibinadamu kwa kwa njia salama.
Imechapishwa:
Katika taarifa ya mkuu wa RSF Mohamed Hamdan Dagalo, maarufu kama Hemedti, amesema hatua hiyo imeafikiwa baada yake kufanya mazungumzo na waziri wa mambo ya kigeni wa Marekani Antony Blinken na mataifa mengine.
"RSF inathibitisha tena kuidhinisha uwekaji silaha chini kwa muda wa saa 24 ili kuhakikisha kuwa raia wanapita salama na kuwahamisha waliojeruhiwa," Hemedti alisema.
Aidha kiongozi huyo wa RSF amelituhumu jeshi la serikali kwa kukosa kutii agizo la kusitishwa kwa vita kwa mujibu wa umoja wa mataifa, akisema kuwa wanajeshi hao wanatuhumiwa kwa kutekeleza mashambulio ya mabomu katika makazi ya raia, hatua inayohatarisha usalama wa watu.
"Hatua hizi ni ukiukaji wa wazi wa misingi na kanuni za sheria za kimataifa na za kibinadamu," aliongeza.
Hata hivyo, Jeshi la Sudan limepuuzilia mbali madai ya wapiganaji wa kijeshi wa RSF kuhusu makubaliano ya siku moja ya kusitisha mapigano yamefikiwa, likitaja hatua hiyo kama propaganda tu.
"Hatujui uratibu wowote na wapatanishi na jumuiya ya kimataifa kuhusu usitishaji vita, na tangazo la waasi la usitishaji mapigano kwa saa 24 linalenga kuficha kushindwa ndani ya saa chache," msemaji wa Jeshi la Sudan alisema katika ukurasa wa twitter wa Jeshi.
"Tumeingia katika hatua mbaya na juhudi zetu zinalenga katika kufikia malengo yake katika ngazi ya utendaji," taarifa ya jeshi inaongeza.
Milio ya risasi ilisikika mjini Khartoum mapema Jumanne asubuhi, huku idadi ya waliofariki ikikaribia 200.
Wakati huu mapigano kati ya pande mbili hasimu za kijeshi yakiingia siku ya nne, idadi kubwa ya raia hawana uwezo wa kupata mahitaji yao muhimu, maduka yakisalia kufungwa.