Kimbunga Freddy: Rais wa Malawi aomba msaada wa kibinadamu kwa taifa lake
Rais wa Malawi Lazarus Chakwera ameiomba Jumuiya ya Kimataifa, kutuma misaada ya kibinadamu katika nchi yake, baada ya kimbunga Freddy, kusababisha vifo vya watu zaidi ya 300 na kuwaacha maelfu bila makaazi.
Imechapishwa: Imehaririwa:
Wakati akitangaza maombolezo ya kitaifa ya wiki mbili, rais Chakwera amesema kiwango cha uharibifu wanachokabiliana nacho ni kikubwa mno kuliko rasilimali walizo nazo.
Malawi imekumbwa na janga, kitu ambacho kimbunga Freddy kimefanya ni kuurudisha nyuma, licha ya ujenzi tuliokuwa tumeanza kuufanya baada ya kutokea majanga yaliyopita,.Naiomba Jumuya ya Kimataifa, tutazameni kwa huruma, tunahitaji msaada kuhakikissha kuwa watu waliookolewa na waliopoteza kil akitu, wapate makaazi, mavazi na chakula
Kimbunga Freddy kimesababisha hadi sasa vifo vya karibu watu 290 katika nchi za Malawi na Msumbiji.
Chakwera ametoa ombi hili, baada ya kutembelea mji mkuu wa Blantyre, ambao umeathiriwa mno na mafuriko makubwa.
Kimbunga hicho cha kitropiki kilianza kuikumba Malawi Jumatatu baada ya kuingia katika Jimbo la Zambezia nchini Msumbiji Ijumaa, na kusababisha mafuriko, maporomoko ya matope na uharibifu uliosababishwa na upepo mkali katika wilaya na miji 12 ya Malawi.
Kwa mujibu wa Idara ya Kukabiliana na Majanga nchini Malawi (DoDMA), katika nchi nzima ya Malawi watu 584 wamejeruhiwa na watu 37 hawajulikani walipo, wakiwemo askari watatu wa kikosi cha uokoaji baada ya boti yao kugonga mti na kupinduka. Ripoti hiyo mpya pia imesema takriban watu 58,946 wameathiriwa, na takriban watu 19,371 kati yao wameyahama makazi yao.