Raila Odinga atangaza maandamano ya amani kuanzia Machi 10
Kiongozi wa upinzani nchini Kenya Raila Odinga, ametangaza maandamano ya amani ya nchi nzima kuanzia Ijumaa, Machi 10, kwa kile anachosema rais William Ruto amekosa kutimiza matakwa ya muungano wa Azimio One Kenya.
Imechapishwa:
Cheza - 00:40
Matakwa haya ni pamoja na kupunguza gharama ya maisha, kukosa kusitisha zoezi la kuwateua makamishna wapya wa Tume ya kitaifa ya Uchaguzi, IEBC, mbali na kukataa kufungua seva, inayohifadhi matokeo ya uchaguzi wa urais wa mwaka uliopita.
Wakenya kuanzia leo watagoma, watafanya maandamano, wataunga pamoja kwa njia ya kuleta mabadiliko katika taifa letu. Tutatumia njia za kikatiba na kisheria. Kwa sababu bwana Ruto amejaribu kununua viongozi wengine, amejaribu kununua mahakama, sasa ni saa ya wakenya kutumia uwezo na nguvu kupitia hiyo katiba yao. Amesema Raila Odinga.
Aidha, Odinga ameitisha pia maandamano makubwa jijini Nairobi tarehe 20 mwezi huu, hatua inayokuja baada ya makataa ya wiki mbili aliyompa Ruto kufanyia kazi matakwa hayo kumalizika jana.
Naye mgombea mwenza katika uchaguzi mkuu uliopita wa Agosti 8, 2022, Martha Karua, amesema serikali iliyoko madarakani si halali, ni ya kidikteta na ni hatari kwa demokrasia ya Kenya.
Rais Ruto, anamshtumu Odinga kwa kutaka kuyumbisha uongozi wake.