Kenyatta atoa wito wa kupelekwa kwa vikosi zaidi DR Congo
NAIROBI – Mratibu wa mazungumzo ya amani kati ya serikali ya Kinshasa na makundi ya waasi, rais wa zamani wa Kenya Uhuru Kenyatta, ameyataka mataifa ya Jumuiya ya Afrika Mashariki kuharakisha mpango wa kutuma wanajeshi wake, Mashariki mwa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo.
Imechapishwa: Imehaririwa:
Cheza - 02:42
Kenyatta ambaye ni mratibu wa mataifa ya Jumuiya ya Afrika Mashariki, kuhusu mzozo wa Mashariki mwa DRC, amesema wanajeshi zaidi wanahitajika ili kudhibiti maeneo ambayo makundi ya waasi wamejiondoa, kwa mujibu wa mkataba wa amani wa Luanda.
Wito huu unakuja wakati huu Uganda na Sudan Kusini, zikisema zinapanga kuwatuma wanajeshi Mashariki mwa nchi hiyo. Mpaka sasa ni Kenya na Burundi tu ndio waliotuma wanajeshi wake mwaka uliopita, kwa mujibu wa makubaliano ya viongozi wa nchi za EAC mwaka uliopita.
Francois Alwande, mchambuzi wa masuala ya DRC anasema Uhuru Kenyatta kama mratibu wa mazungumzo ya kupatikana kwa amani nchini DRC yuko na haki ya kutoa kauli ya kutaka wanajeshi zaidi kupelekwa eneo la mashariki.
"Kuna yale matatizo ya ndani kwamba raia wa Congo hawana imani tena na jeshi hilo, jeshi hilo wakati liliundwa lilipewa majukumu ya kwenda kupambana na waasi wenye silaha."ameeleza Francois Alwande.
Aidha, amesema anasikitishwa ripoti za kuendelea kwa mapigano kati ya wanajeshi wa DRC na waasi wa M 23 katika jimbo la Kivu Kaskazini, licha ya kuwepo kwa wito wa utulivu, kama ilivyokubaliwa na marais wa Jumuiya ya Afrika Mashariki waliokutana jijini Bujumbura, wiki iliyopita.
Kenyatta pia ametaka waasi na serikali ya DRC kutekeleza makubaliano ya mazungumzo ya amani yaliyofanyika jijini Nairobi mwaka uliopita na kutoa wito kwa msaada wa haraka wa kibinadamu kwa maelfu ya watu waliokimbia makwao kwa sababu ya vita.