Shule zafunguliwa tena Malawi
Masomo yamerejelewa tena kwa shule za msingi na sekondari katika miji miwili mikubwa nchini Malawi, baada ya kuwa zilifungwa kutokana na msambao wa ugonjwa wa kipindupindu.
Imechapishwa: Imehaririwa:
Shule katika mji mkuu Lilongwe na ule wa kibiashara Blantyre, zilikuwa zimefungwa kwa zaidi ya wiki mbili baada ya sikukuu ya Christmas, ambapo wanafunzi kadhaa waliripotiwa kuambukizwa.
Ugonjwa wa kipindupindu ambao uliripotiwa nchini Malawi tangu mwezi Machi mwaka jana, umeshaua watu zaidi ya 700, huku maambukizo yakiripotiwa kuwa ya kiwango cha juu kwenye miji hiyo.
Katika taarifa yake, waziri wa afya, Khumbize Chiponda, amesema uamuzi wa kufunguliwa kwa shule hizo, umekuja baada ya timu yake kujiridhisha kuna miundombinu ya maji safi na salama.
Nchi ya Malawi ni miongoni mwa mataifa 31 duniani ambayo yameripoti uwepo wa kipindupindu.