Tunisia kukumbwa na mgomo wa wafanyakazi
Muungano wa wafanyakazi nchini Tunisia, umetangaza mgomo wa nchi nzima hivi leo, kushinikiza nyongeza ya mshahara, ikiwa ni shinikizo kwa rais Kais Saied ambaye ameshtumiwa kwa kuwatenga wanasiasa wa upinzani, kwenye mazungumzo ya kitaifa.
Imechapishwa:
Mgomo huu unatarajiwa kusitisha shughuli kwenye mashirika na kampuni za umma 159 kwa kile viongozi wa wafanyazi wanasema wanapigia haki zao za kiuchumi.
Mgomo huo wa wafanyakazi wa serikali umeanza katika hali ambayo, Tunisia kwa siku kadhaa sasa imekuwa ikishuhudia maandamano ya wananchi wakilalamikia utendaji wa serikali na hali mbaya ya uchumi nchini humo.
Nchi hiyo iko chini ya mashinikizo ya Mfuko wa Fedha Duniani IMF unaoitaka isimamishe mishahara ya wafanyakazi wa sekta za umma, kama sehemu ya mageuzi ya kujaribu kupunguza nakisi ya bajeti ya nchi.
Nchi wafadhili zimetishia kuacha kuusaidia uchumi wa Tunisia, ambao unayumba na kukabiliwa na mgogoro mkubwa toka aondolewe madarakani dikteta wa zamani wa nchi hiyo, Zainul Abiddin Ben Ali mwaka 2011.