DRC: Baraza la Mawaziri lajaribu kutatua mgogoro wa mafuta
Huko Kinshasa, mji mkuu wa DRC, foleni ndefu katika vituo vya mafuta zinaelekea kupungua. Hali si ya kutisha kuliko mwanzoni mwa wiki, wakati nchi inakabiliwa na uhaba wa mafuta. Serikali inatafuta suluhu.
Imechapishwa:
Mikutano imeongezeka wiki nzima kati ya makampuni ya mafuta na serikali kutafuta suluhu na kuepuka uhaba wa bidhaa hiyo katika maghala kwa sababu mgogoro huu una athari za moja kwa moja kwa fedha za umma. Katika wiki mbili zilizopita pekee, karibu dola milioni 100 zimetolewa kulipa madeni ambayo Serikali inadaiwa na makampuni ya mafuta katika muktadha wa ruzuku katika sekta ya hidrokaboni.
Umakini katika usimamizi wa fedha za umma
Wakati wa mkutano wa Baraza la Mawaziri siku ya Ijumaa, Waziri Mkuu Jean-Michel Sama Lukonde alipendekeza sana tahadhari katika usimamizi wa fedha za umma ili kuweka uwezo katika kukabiliana na athari zisizotarajiwa za mgogoro huo. Aidha, athari ya mgogoro huu unaweza kuonekana, hata katika kiwango cha muundo wa bei ya bidhaa za petroli. Majadiliano yanaendelea kwa ajili ya marekebisho ya juu.
Waziri Mkuu Jean-Michel Sama Lukonde alizungumzia usumbufu ambao alisema unahatarisha moja kwa moja bei ya vyakula pamoja na gharama za usafiri.
Kuongeza uzalishaji
Wakati huo huo, serikali inasema pia inataka kutoa suluhisho la muda mrefu. Hivyo ilipitisha mradi wa kuzindua mwito wa zabuni za ugawaji wa vitalu kumi na sita vya mafuta kote nchini. Lengo ni kuboresha mapato ya serikali na kuongeza uzalishaji wa mafuta kitaifa.
Nchi inataka kuzidisha uzalishaji wake wa sasa wa mapipa 26,000 tu kwa siku. Kamati ya dharura itaundwa kwa madhumuni haya.