Morocco: Serikali mpya yatangazwa
Mohammed VI, Mfalme wa Morocco, ametangaza serikali yake mpya tangu Alhamisi wiki hii akiwa pamoja na Waziri wake Mkuu Aziz Akhannouch, mshindi wa uchaguzi wa wabunge wa mwezi Septemba na chama chake cha mrengo wa kulia, RNI (Rally National of Independents).
Imechapishwa:
Hakuna mabadiliko yaliyofanyika kwenye wizara kuu kama Wizara ya Mambo ya Ndani ambayo inasimamiwa na Abdelouafi Laftit na hasa Wizara ya Mambo ya Nje. Nasser Bourita ameendelea kushikilia wadhifa wake katikati mwa mivutano ya kikanda, hasa na Algeria na Uhispania.
Chama cha RNI, ambacho mwezi uliopita kilimaliza miaka 10 ya utawala wa Kiislamu kwenye Baraza la Wawakilishi - na hivyo kushinda viti 102 kati ya 395 - kinashikilia wizara za utalii na afya.
Baraza hili jipya la mawaziri linaundwa na mawaziri 24, wakiwemo wanawake saba dhidi ya wanne katika serikali iliyopita.
Serikali ya Akhannouch hata hivyo italazimika kukamilisha mpango kabambe wa chanjo ya jumla ya matibabu inayotakiwa na mfalme ifikapo mwaka 2025.