Askari 15 wa kulinda amani kutoka Tigray wakataa kurudi Ethiopia
Maafisa wa umoja wa mataifa wamesema wanajeshi 15 wa jeshi la kulinda la umoja wa mataifa huko Ethiopia waliotorokea nchini Sudan Kusini, na ambao wengi wao ni wazaliwa kutoka jimbo la Tigray, wamekataa kurejea Ethiopia.
Imechapishwa:
Katika taarifa yake kwa vyombo vya habari, umoja wa Mataifa umethibitisha hilo huku likisema kuwa ni haki yao kuomba hifadhi kama wanahofia maisha yao.
Akizungumza wakati wa mkutano na waandishi wa habari jumanne ya tarehe 23 februari, msemaji wa umoja wa mataifa Stephane Dujarric amesema wanajeshi 169 wa kikosi cha kulinda amani walitoka Ethiopia walitarajiwa kuondoka Juba ili kubadilishwa na wanajeshi wapya kama sehemu ya mzunguko wa kawaida wa wanajeshi hao.
Taarifa zinasema askari hao 15 waliokataa kupanda ndege kurudi nyumbani wameomba kubaki nchini humo kuanzisha utaratibu wa kuomba hifadhi, na kwamba huku umoja wa mataifa ukisema kuwa wanapewa msaada na Wizara ya Mambo ya nje ya Sudan Kusini.
Shirika la Umoja wa Mataifa la kuwashughulikia wakimbizi - UNHCR limesema linafahamu suala hilo na linawasiliana na mamlaka za Sudan Kusini.