Ebola: Mataifa jirani na Guinea yaanza kuchukua hatua za tahadhari
Siku mbili baada ya Guinea kutangaza kesi saba za maambukizi ya virusi vya Ebola, Kusini mwa nchi, nchi jirani zimeanza kuchukuwa hatua za tahadhari kuzuia kusambaa kwa ugonjwa huo hatari.
Imechapishwa:
Siku ya Jumapili rais wa Liberia George Weah alitangaza kuziweka mamlaka za afya za nchi hiyo katika kiwango cha juu cha tahadhari baada ya watu watatu kufariki dunia kwa ugonjwa wa Ebola kwenye nchini Guinea.
Waziri wa Afya wa Guinea Remy Lamah alithibitisha kuwa watu watatu walifariki dunia kutokana na Homa ya Ebola, ikiwa ni vifo vya kwanza vya maradhi hayo tangu kutokea mlipuko mkubwa wa mwaka 2013 hadi 2016.
Ugonjwa wa Ebola uliua watu 1,000 katika nchi za Guinea, Liberia na Sierra Leone.
Ugonjwa utokanao na kirusi cha Ebola ni ugonjwa hatari wenye uwezo wa kusababisha kifo kwa asilimia 90. Shirika la afya duniani, WHO katika tovuti yake (https://www.who.int/) inasema kwa mara ya kwanza ulibainika mwaka 1976 huko Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo, DRC na Sudan.
Chanzo cha kirusi hiki hadi sasa hakijulikani lakini popo aina ya (Pteropodidae) wanaonekana kuwa wabebaji wa kirusi hicho, kwa mujibu wa ushahidi uliopo sasa.
Kulingana na wadadisi wa masuala ya afya, Ebola ni ugonjwa unaosabibishwa na virusi vya homa ya hemoraji (yaani "kutokwa na damu sana").
Ina kiwango cha juu cha uambukizaji; watu wengi wanaweza kuambukizwa haraka. Huo ugonjwa wa damu kutoganda unaua sana: kati ya watu 10 waliopata virusi vya Ebola, basi wastani kati ya 5 na 9 hufa.
Ebola haina chanjo wala tiba lakini kupokea matibabu katika vituo vya Ebola mapema huongeza uwezekano wa kupona.