HRW: Mashambulizi Tigray yameuwa raia wasiopungua 80
Jeshi la Ethiopia limewauwa raia wasiopungua 83 na kusababisha maelfu ya watu kuyatoroka makaazi yao baada ya kutekeleza mashambulizi ya angani katika maeneo yenye watu wengi katika wiki za kwanza za mapigano ili kuwaondoa mamlakani viongozi walioasi katika jimbo la Tigray, shirika la kimataifa la haki za binadamu la Human Rights Watch (HRW) limebaini.
Imechapishwa:
Mashambulio makubwa ya majeshi ya serikali ya Addis Ababa yaliyotumia silaha za kivita" yaliharibu nyumba, hospitali, shule na masoko," kulingana na ripoti ya shirika la HRW ambayo imejikita na hali katika miji mitatu: mji mkuu wa mkoa Mekele, Shire na Humera.
"Mwanzoni mwa mapigano hayo, vikosi vya serikali kuu ya Addis Abeba vilitekeleza mashambulizi kiholela katika maeneo ya miji ya Tigray, ambayo inaonekana yayalisababisha vifo vya watu kadhaa na kuwajeruhi wengine," amesema Laetitia Bader, mkurugenzi wa HRW katika eneo la Pembe la Afrika.
Ethiopia "inapaswa kuidhinisha haraka uwepo wa waangalizi wa Umoja wa Mataifa huko Tigray kuchunguza tabia za pande zilizohusika katika mzozo huu ambao umeharibu maisha ya mamilioni ya watu," ameongeza.
Waziri Mkuu wa Ethiopia na mshindi wa Tuzo ya Amani ya Nobel ya mwaka 2019 Abiy Ahmed alitangaza mwishoni mwa mwezi Novemba, wakati jeshi la shirikisho lilichukua udhibiti wa mji mkuu wa mkoa Mekele, kumalizika rasmi kwa operesheni ya jeshi iliyozinduliwa mwanzoni mwa mwezi huo huo kuwaondoa mamlakani viongozi walioasi katika jimbo la Tigray.
Lakini mashirika ya kibinadamu na wanadiplomasia wanasisitiza kuwa ukosefu wa usalama katika jimbo hilo bado unazuia sana shughuli za kibinadamu.