Umoja wa Mataifa wataka 'mapigano kusitishwa' Libya
Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa limeidhinisha, kwa mara ya kwanza tangu kuzuka kwa mgogoro nchini Libya, azimio likitaka pande husika kufikia "makubaliano ya kudumu ya kusitishwa mapigano" katika nchi hii inayokabiliwa na vita vya wenyewe kwa wenyewe.
Imechapishwa:
Mwezi Januari mwaka huu pande zinazokinzana nchini Libya zilifikia mkataba wa kusitisha mapigano, lakini mkataba huo unalegalega kutokana na kuwa mapigano yamekua yakiendelea na kila upande ukishutumu upande mwengine kukiuka mkataba huo.
Nakala hiyo, iliyoandaliwa na Uingereza, imepitishwa kwa kura 14 kati ya 15, huku Urusi ikijizuia.
Azimio hilo limepitishwa baada ya mazungumzo yaliyodumu zaidi ya wiki tatu, huku kukionekana mgawanyiko wa kimataifa unaoendelea licha ya kuonyesha umoja wao katika mkutano uliofanyika katika mji mkuu wa Ujerumani, Berlin, Januari 19; Mkutano ambao walishiriki marais wa Urusi na Uturuki ambao kila mmoja anaunga mkono kambi moja hasimu nchini Libya.
Azimio hilo "linataka kuepo na haja ya kueopo na makubaliano ya kudumu ya kusitisha mapigano nchini Libya, kabla ya yote na bila masharti".
Urusi inashtumiwa kwa miezi kadhaa kuunga mkono usafirishaji wa maelfu ya mamluki wa kundi la Wagner, linalodaiwa kuwa na uhusiano wa karibu na ikulu ya rais wa Urusi, kwenda nchini Libya kumsaidia Marshal Khalifa Haftar ambaye amekuwa akitafuta tangu Aprili 4, 2019 kudhibiti kijeshi mji wa Tripoli ambapo ni makao makuu ya Serikali ya umoja wa kitaifa (GNA) ya Fayez al-Sarraj, inayotambuliwa na Umoja wa Mataifa.
Hata hivyo Moscow imekanusha kuhusika kwake katika usafirishaji wa mamluki wa Urusi kwenda nchini Libya.