Pata taarifa kuu
DRC-USALAMA

Mpango mpya wa kumaliza mapigano Kivu Kusini kujadiliwa DRC

Jitihada zinaendelea kuongezeka kwa lengo la kuzuia mapigano katika Mkoa wa Kivu Kusini, Mashariki mwa DRC, haswa katika maeneo ya bonde la Ruzizi na Fizi. 

Katika mkoa wa Kivu Kusini, mashariki mwa nchi, uhasama kati ya makabila unaendelea kuripotiwa. Hapa ni katika Jimbo la Fizi.
Katika mkoa wa Kivu Kusini, mashariki mwa nchi, uhasama kati ya makabila unaendelea kuripotiwa. Hapa ni katika Jimbo la Fizi. © AFP PHOTO/FEDERICO SCOPPA
Matangazo ya kibiashara

Makundi yenye silaha kutoka nchi za kigeni na yale yanayoundwa na raia wa DRC yanaendelea kujidhatiti katika maeneo hayo na kusababisha mvutano kati ya jamii. Kutokana na hali hiyo viongozi wanaandaa kuanzisha mazungumzo yatakayojumuisha wadua mbalimbali, ikiwa ni pamoja na wanaharakati wa mashirika ya kiraia, kwa mujibu wa vyanzo kadha vya serikali.

Jumamosi wiki iliyopita, mbunge Norbert Basengizi Katintima, ambaye ni miongoni mwa viongozi wa mkoa huo wanaopendekeza mazungumzo hayo, alimpa Waziri Mkuu ripoti yake, uchambuzi wa kurasa nne ambapo alitoa mapendekezo kadhaa kwa serikali. Mbunge Norbert Basengizi Katintima, naibu mwenyekiti wa zamani wa Tume ya Uchaguzi, anadai kuwa ni msemaji wa wanyonge kutoka jamii kumi na tatu za Mkoa wa Kivu Kusini ambapo anatokea.

Mapendekezo yake yanalenga kumaliza uhasama kati ya makabila sita miongoni mwa makabila hayo, ikiwa ni pamoja na Wanyamulenge, Wafuliru, Wanyindu, Wavira na Warundi. Kila moja ya makabila hayo kwa sasa yana kundi lake lenye silaha. Makabila haya yanatakiwa kuhamasishwa kuweka chini silaha. Kwa kufanikisha hilo, kunatakiwa kuundwa kwa kamati ya ufuatiliaji wa operesheni ya upokonyaji silaha na kuwarejesha katika maisha ya kiraia. Na ikiwa makundi haya yatakubali, watapaswa kushirikishwa katika mazungumzo mapya ambayo hayatakuwa tu kati ya jamii, lakini chini ya kivuli cha serikali, Norbert Basengizi Katintima amependekeza.

Norbert Basengizi Katintima pia amependekeza serikali ya DRC kuanzisha mazungumzo na nchi jirani, ikiwa ni pamoja na Rwanda na Burundi, nchi zinazoshutumiwa kuchochea vita katika eneo hili la DRC kwa kuyafadhili makundi yenye sialaha yanayoundwa na raia wa DRC na yale yanayoundwa na raia kutoka nchi hizo.

Hata hivyo wanaharakati wa mashirika ya kiraia wamefutilia mbali mapendekezo hayo ya Norbert Basengizi Katintima kama msimamizi wa mazungumzo kati ya jamii hizo kumi na tatu, wakikumbusha uhalifu, hasa mauaji aliofanya katika mkoa huo alipokuwa katika kundi la zamani la waasi la RCD.

Kusambaza :
Ukurasa haipatikani

Maudhui unayojaribu kuyatafuta hayapatikani kwa sasa au yamekwishaondolewa.