Polisi watumwa katika maeneo mbalimbali kukabiliana na waandamanaji Algeria
Nchi ya Algeria inaendelea kukumbwa na maandamano licha ya rais wa nchi hiyo Abdelaziz Bouteflika kuchukuwa hatua ya kujiuzulu kwa shinikizo la maandamano.
Imechapishwa:
Leo Ijumaa maeneo mbalimbali ya nchi hiyo yanatarajia kukumbwa na maandamano makubwa.
Wananchi wa Algeria wanajiandaa kushiriki maandamano ya Ijumaa ya nane, huku polisi wakiapa kukabiliana na waandamanaji.
Waandamanaji wanaendelea kuomba kujiuzulu kwa utawala mzima wa Bouteflika.
Siku ya Alhamisi usiku, polisi wa kuzima ghasia walionekana wengi kuliko maandamano ya kwanza wakijielekeza kwenye eneo la Posta kuu katikati mwa mji wa Algiers.
Vikosi vya usalama vimeweka vizuizi barabarani, hasa kwenye barabara zinazoelekea mji mkuu Algiers.
Hii ni Ijumaa ya kwanza ya maandamano tangu kuteuliwa kwa Abdelkader Bensalah kama rais wa mpito wa Algeria. Bw Bensalah ni rafiki wa karibu wa Abdelaziz Bouteflika ambaye anajaribu kutuliza hasira ya wananchi wa Algeria.
Hata hivyo waandamanaji wanataka kiongozi huyo, naye pia aweze kujiuzulu.
Kwa siku kadhaa, Mkuu wa majeshi Ahmed Salah amekuwa akijaribu kutuliza hasira ya waandamanaji, bila mafanikio.
Tukisema hapana ni hapana, wamesema waandamanaji: "Hatukumfukuza Bouteflika ili kumrejesha mshirika wake wa karibu".
Maandamano yameendelea kushuhudiwa kila kukicha wiki hii.