Kinshasa yaomba Umoja wa Mataifa kujiweka kando na masuala ya DRC
Joto la kisiasa linaendelea kuongezeka nchini Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo siku sita kabla ya uchaguzi uliopangwa kufanyika Desemba 23. Serikali ya DRC imeendelea na msimamo wake wa kufutilia mbali msaada wowote kutoka washirika wake wa Magharibi na Umoja wa Mataifa na ujumbe wowote wa waangalizi kutoka nchi za Magharibi.
Imechapishwa:
Serikali ya DRC inasema kuwa itatumia ndege na helikopta za Umoja wa Mataifa nchini humo (MONUSCO) kwa kusafirisha vifaa vya uchaguzi nchini kote, (nchi yenye ukubwa wa kilomita mraba milioni 2.3, na mipaka tisa) ambayo ina kilomita 3,400 tu ya barabara za lame.
"Tumechukuwa uamuzi huo kwa sababu sisi sio waomba omba. Kwa kweli DRC, ina matatizo, lakini pia ni nchi ya wanaume na wanawake wenye busara na ambao wana majukumu makubwa ya kuiendeleza," Rais Joseph Kabila ameliambia gazeti la Ubelgiji la kila siku la Le Soir.
Katika nchi hii, ambayo ni kubwa sawa na Ufaransa zaidi ya mara nne na Ubelgiji zaidi ya mara 80, gharama ya uchaguzi wa urais, wa wabunge na wa magavana inakadiriwa kuwa dola milioni 500, sawa na 10% ya bajeti ya kila mwaka ya Serikali.
Serikali ya DRC inakataa ujumbe wowote wa waangalizi wa uchaguzi kutoka Marekani au Umoja wa Ulaya (EU).
Waangalizi zaidi ya mia moja kutoka Afrika ndio wameruhusiwa kufanya uchunguzi katika vituo 80,000 vya kupigia kura ambapo wapiga kura milioni 40 watashiriki uchaguzi huo.
Mgombea wa upinzani Martin Fayulu ameendelea kutoa wito kwa "jumuiya ya kimataifa" baada ya kampeni zake kugubikwa na vurugu zilizosababishwa na vikosi vya usalama, huku wafuasi wake wanne wakiuawa na polisi kwa mujibu wa vyanzo kadhaa.
Serikali ya DRC imeomba Umoja wa Mataifa kutoingilia kati katika masuala ya DRC, wakati Umoja huo una moja ya ujumbe mkubwa duniani nchini humo tangu mwaka 1999.
Katika miezi kumi na miwili iliyopita, Walinda amani 27 wameuawa nchini DRC, Monusco imesema katika taarifa yake.