Wanahabari kadhaa watoweka katika mazingira ya kutatanisha ukanda wa Maziwa Makuu
Wanahabari kutoka mataifa ya ukanda wa Maziwa Makuu wapo katika orodha ya wale wanaoendelea kudhulumiwa na hatua kutochukuliwa. Baadhi yao wametishiwa, kufungwa na kutoweka katika mazingira ya kutatanisha.
Imechapishwa:
Mashirika ya kimataifa ya kutetea haki za Wanahabari Reporters Sans Frontières, RSF na Kamati inayowashughulikia Wanahabari Committe to Protect Journalists (CPJ) wanaendelea kushinikiza kupatikana kwa Wanahabari ambao hawaonekani waliko.
Hii ni orodha ya Wanahabari kutoka Afrika Mashariki na Kati ambao hawajulikani waliko.
Manasse Mugabo
Alikuwa Mkurugenzi wa Redio ya Umoja wa Mataifa kuhusu Rwanda NAMIR.
Aliondoka jijini Kigali kwenda nchini Uganda mwezi Agosti mwaka 1995 kwenda kwa mapumziko binafsi, lakini haifahamiki alipotelea wapi.
Acquitté Kisembo
Kisembo, hadi kutoweka kwake, alikuwa ni Mwanafunzi wa Udaktari lakini alikuwa akishirikiana na Shirika la Habari la Agence France-Presse (AFP) katika jimbo la Ituri, nchini DRC.
Alitoweka mwaka 2003, na mtu wa mwisho kumuona ni Anthony Morland, Mwahababari wa AFP aliyekuwa anafanya naye kazi.
Inaaminika kuwa waasi wa UPC ndio waliomteka na kumuua.
Azory Gwanda
Mwanahabari kutoka nchini Tanzania. Alipotea mwezi Novemba mwaka 2017. Alikuwa anaripotia Gazeti la kibinafasi la Mwananchi na The Citizen.
Mkewe Anna Pinoni alisema watu wanne ambao hakuwafahamu walimchukua mume wake akiwa katika kitongoji cha Kibiti.
Hadi kutoweka kwake, alikuwa anaripoti kuhusu hali ya usalama katika Wilaya ya Kibiti iliyokuwa inashuhudia kuuawa kwa maafisa wa polisi na wawakilishi wa serikali.
Haifahamiki waliomteka na nia yao.
Emmanuel Munyemanzi
Mkuu wa kitengo cha uzalishaji wa vipindi katika Televisheni ya Taifa, alitoweka mwaka 2003.
Ripoti zinasema kuwa alikuwa njiani kwenda kazini jijini Kigali lakini hakufika Ofisini.
Miezi miwili kabla ya kutoweka kwake, Mkurugenzi wa Tume ya Mawasiliano alimshtumu Mwanahabari huyo kwa kusababisha hitilafu ya kimtambo wakati wa kurekodi mjadala wa kisiasa.
Kumekuwa na ripoti ambazo hazijathibitishwa kuhusu kupatikana kwa mwili wake.
Jean Bigirimana
Jean Bigirimana, ni ripota wa Gazeti la kibinafsi la Iwacu nchini Burundi.
Alikuwa pia anafanya kazi na kituo cha Redio cha Rema FM. Aliondoka nyumbani kwake jijini Bujumbura, tarehe 22 mwezi Julai mwaka 2016 baada ya kupigiwa simu kutoka kwa Shirika la ujasusi.
Shirika la Associated Press liliripoti kuwa alikamatwa na maafisa wa Inteljensia. Kuna hofu kuwa aliuawa.
Alikuwa miongoni mwa mamia ya Wanahabari waliotorokea nchini Rwanda baada ya jaribio la mapinduzi mwaka 2015.