Wafanyakazi wa wizara ya afya, mashariki mwa DRC wapewa likizo ya muda
Wizara ya afya nchini Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo imewapa likizo ya muda wafanyikazi 74 katika kituo cha afya cha Mangina kwa sababu ya kuwa karibu na wagonjwa walioambukizwa ugonjwa hatari wa Ebola, Mashariki mwa nchi hiyo.
Imechapishwa:
Maafisa wa serikali nchini humo wamesema, wafanyikazi hao wametengwa kwa muda wa siku 21, ili kubainika iwapo watakuwa ameambukizwa Ebola kwa sababu kuna baadhi yao waliwagusa watu walioambukuzwa.
Katika kipindi hicho chote, watalazimika kusalia katika eneo moja, hadi watakapobainika kuwa hawana maambukizi yoyote kabla ya kurejea kazini na kutangamana na watu wengine.
Aidha, Wizara ya afya nchini humo imetenga vituo vitatu katika miji ya Mabalako, Beni, na Oicha kuwasaidia watu wanaoshukiwa kuambukizwa.
Kuanzia mwezi huu, watu zaidi ya 10 wamepoteza maisha na wengine zaidi ya 20 kuambikizwa ugonjwa huu hatari.