Takribani watu 14 wauawa katika shambulizi mjini Mogadishu Somalia
Takribani watu 14 wameuawa katika mashambulizi ya mabomu ya kutegwa garini katika hoteli kwenye mji wa Mogadishu nchini Somalia jana Jumamosi , mashambulizi yanayodaiwa kutekelezwa na kundi la Al Shabab.
Imechapishwa:
Kufuatia milipuko mashahidi wanasema walisikia milio ya risasi katika Hoteli ya Nasa Halbod ambayo ilifungwa na vikosi vya usalama huku wanamgambo wakidaiwa kuwa ndani.
Afisa wa usalama, Mohammed Moalim Adan amesema kuwa watu takribani 14 wamethibitishwa kuuawa wengi wao raia na vikosi vya usalama vinaendelea kufanyakazi kuhakikisha eneo hilo linakuwa salama.
Shambulizi hili limetokea wiki mbili baada ya shambulizi kubwa zaidi na baya kuwahi kushuhudiwa nchini Somalia, na kuua watu takribani 358, na kulifanya kuwa shambulio la hatari zaidi katika historia ya nchi hiyo.
Kundi la Al Shabaab kimekiri kuhusika na shambulizi la jana Jumamosi katika taarifa yake kupitia kituo cha redio cha Andalus.