UNHCR yashuhudia ukiukaji mkubwa jimboni Kasai DRC
Umoja wa Mataifa jana Ijumaa umeonya kuwa wafanyakazi wake wameshuhudia uharibifu na mateso kwa "kiasi kikubwa" katika mkoa wa Kasai nchini Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo.
Imechapishwa:
Wafanyakazi kutoka shirika la wakimbizi la Umoja wa Mataifa UNHCR walirejea juma lililopita kutoka jimbo la Kamonia kwenye mpaka wa nchi ya DRC na Angola na wameshuhudia "vijiji vilivyoteketezwa kwa moto na watu wakiwa katika hali mbaya, ameeleza msemaji Cecile Pouilly mbele ya waandishi wa habari huko Geneva.
Aidha hapo jana Ijumaa UNHCR imezitaka mamlaka kuruhusu mashirika ya misaada ya kibinadamu kufika kikamilifu katika maeneo yenye uhitaji na kuwafikia wanaohitaji ulinzi na msaada.
Ujumbe huo ni wa kwanza kutoka UNHCR kufika katika eneo hilo ambalo huduma za kimsingi zimekoma kabisa na uhalifu unaendelea alisema Pouilly.
Vurugu huko Kasai zilizuka mwezi Septemba mwaka jana baada ya kifo cha kiongozi wa kikabila, aliyejulikana kama Kamwina Nsapu, ambaye aliasi dhidi ya mamlaka ya serikali ya Rais Joseph Kabila huko Kinshasa na wawakilishi wake wa serikali za mtaa.