Kipindupindu chaua watu wanne Mashariki mwa DRC
Serikali ya jimbo la Kivu kaskazini mashariki mwa Jamhuri ya kidemokrasia ya Congo imesema watu wanne ndio waliopoteza maisha kutokana na ugonjwa wa kipindupindu na makumi wengine kulazwa hospitalini katika wilaya ya Nyiragongo.
Imechapishwa: Imehaririwa:
Hata hivyo, taarifa iliyotolewa na Mashirika ya kiraia, inasema kuwa watu waliopoteza maisha ni kumi na wawili, tangu kuzuka kwa ugonjwa huo mwishoni mwa wiki iliyopita, na kwamba wagonjwa zaidi ya 100 wamelazwa hospitalini mjini Goma.
Madaktari wanasema ukosefu wa maji salama ya kunywa na matumizi ya nyumbani katika maeneo mengi Mashariki mwa nchi hiyo, yamesababisha kuenea kwa kwa kipindupindu.
Daktari Marsial Kambumbu amabye pia ni Waziri wa afya katika serikali ya Jimbo la Kivu kaskazini ameimbia RFI Kiswahili kuwa serikali, inafanya kilicho ndani ya uwezo wake kuhakikisha kuwa maambukizi haya hayaripotiwi tena.
Kambumbu amewataka raia wa eneo hilo kuhakikisha kuwa wanachemsha maji kabla ya kunywa lakini pia kunawa mikono baada ya kutoka chooni na kabla ya kula chochote.