Mwili wa Etienne Tshisekedi kurejeshwa DRC kutoka Ubelgiji
Mwezi mmoja baada ya kifo cha Etienne Tshisekedi nchini Ubelgiji, makubaliano kuhusu mazishi yake yamepatikana. familia ya mwanasiasa huyo wa upinzani nchini DR Congo imetangaza kwamba mwili wake utasafirishwa kuelekea mjini Kinshasa Jumamosi Machi 11.
Imechapishwa:
Mwanasiasa huyo wa kihistoria wa upinzani Etienne Tshisekedi alifariki mjini Brussels Februari 1 akiwa na umri wa miaka 84. Mwili wake hatimaye utarejeshwa nchini Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo Machi 11 kufuatia makubaliano yaliyofikiwa kuhusu mazishi, Askofu Gerard Mulumba Kalemba, ndugu wa Etienne Tshisekedi, ameiambia RFI.
"Jumamosi, Machi 11 ni siku teule kwa kuurejesha kwa ndege mwili wa Etienne Tshisekedi mjini Kinshasa. Na bado hatujakua na taarifa zaidi kwa kile kilichopangwa kuhusu mazishi yake mjini Kinshasa. Kwanza Mwili wake utawekwa mbele ya makao makuu ya Bunge kwa kuruhusu wabunge na viongozi wengine serikalini kutoa heshima zao za mwisho, kabla ya mazishi. Tulishauriana na kukubali sehemu iliyochaguliwa na Bw Kimbuta, gavana wa mji wa Kinshasa. Tulichagua maeneo mengine, lakini hakuyakubali, aliyakata. Sehemu hiyo tuliikubali baada ya majadiliano mengi. Hatimaye, tulikubali na kusema atazikwa hapo kwa muda. Baadaye, tunafikiria kutafuta sehemu nyingine ambayo atazikwa, na hapo ndipo kutajengwa sanamu lake au mnara wa kumbukumbu", Askofu Gerard Mulumba Kalemba amesma .