Pata taarifa kuu
GAMBIA-ICC

Gambia yawa nchi nyingine ya Afrika kujitoa mahakama ya ICC

Nchi ya Gambia imekuwa ni taifa jingine la Afrika kutangaza kujitoa kwenye mahakama ya kimataifa ya uhalifu wa kivita ya ICC, ikiituhumu mahakama hiyo kwa kuwalenga viongozi wa Afrika peke yake.

Rais wa Gambia, Yahya Jammeh akihutubia kwenye umoja wa Mataifa, 27 September 2013.
Rais wa Gambia, Yahya Jammeh akihutubia kwenye umoja wa Mataifa, 27 September 2013. UN Photo/Amanda Voisard
Matangazo ya kibiashara

Uamuzi huu wa taifa masikini kwenye ukanda wa Afrika Magharibi, inafuatia uamuzi kama huo uliofanywa na Serikali ya Burundi na Afrika Kusini ambazo juma lililopita zilitangaza kujiondoa kwenye mahakama hiyo iliyoanzishwa kuwashtaki wahalifu wa kivita.

Uamuzi wa Banjul, unaelezwa kuwa ni pigo kwa mahakama hiyo pamoja na ofisi ya mwendesha mashtaka Fatou Bensouda, raia wa Gambia ambaye pia aliwahi kuwa waziri wa sheria wa nchi hiyo.

Waziri wa habari wa Gambia, Sheriff Bojang ndiye aliyetoa tangazo hilo kupitia televisheni ya taifa, ambapo amesema mahakama hiyo imekuwa ikiwalenga viongozi wa Afrika peke yake na kuwaacha viongozi kutoka nchi za Magharibi.

Kwenye taarifa yake alitolea mfano kesi dhidi ya waziri mkuu wa zamani wa Uingereza Tony Blair, ambaye mahakama hiyo iliachana na mpango wa kumfungulia mashtaka kutokana na kuhusika kwake kwenye vita ya Iraq.

“Kuna nchi nyingi sana za magharibi, angalau 30, ambazo viongozi wake wametekeleza makosa ya uhalifu wa kivita dhidi ya mataifa huru na watu wake toka mahakama hiyo ilipoundwa, lakini hakuna kiongozi hata mmoja ambaye amepelekwa mbele ya mahakama hiyo”. Alisema waziri huyo.

Mahakama ya ICC, iliyoanzishwa mwaka 2002 mara nyingi imekuwa ikituhumiwa kwa kuwa na upendeleo dhidi ya viongozi wa nchi za magharibi na badala yake inawalenga viongozi wa Afrika peke yake.

Nchi ya Gambia, mara kadhaa imejaribu kutumia mahakama hiyo kuushtaki umoja wa Ulaya kwa kuhusika na vifo vya mamia ya raia wake waliokufa kwenye bahari ya mediterania bila mafanikio.

Kusambaza :
Ukurasa haipatikani

Maudhui unayojaribu kuyatafuta hayapatikani kwa sasa au yamekwishaondolewa.