Upinzani DRC wafanya mgomo nchi nzima kupinga kuanza kwa mazungumzo
Muungano wa vyama vya upinzani nchini Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo, DRC, umeitisha mgomo wa nchi nzima, kupinga hatua ya mpatanishi wa mzozo wa kisiasa nchini humo Edem Kodjo kuitisha kamati ya maandalizi ya mazungumzo hayo kuanza vikao, kinyume na makubaliano yao ya awali.
Imechapishwa:
Upinzani unataka kwanza kabla ya kufanyika kwa mazungumzo hayo, wafungwa wa kisiasa waachiwe huru pamoja na kufutwa kwa kesi zote za kisiasa.
Miezi michache iliyopita, mpatanishi Kodjo alikutana na makundi mbalimbali ya kisiasa nchini DRC, ambayo katika masharti yao, walitaka kwanza wafungwa wote wa kisiasa waachiwe huru pamoja na kufuta kesi zote zinazodaiwa kuwa za kisiasa
Katika muktadha huo, Rais Kabila tayari ameanza kutoa msamaa kwa baadhi ya wafungwa, hatua ambayo inazungumziwa na wapinzani kuwa finyu ikizingatiwa idadi yao kwa maana kwamba kati ya wafungwa mia moja wanne pekee ndio ambao wamepewa msamaha huo.
Katika mvutano uliopo, Kanisa Katoliki imeingilia kati na kuwaomba wanasiasa kuweka mbele maslahi mapana ya taifa.
Hata hivyo, bado msuguano unaendelea kwa vile Tshisekedi na washirika wake wanaendelea kushinikiza kuondoka kwa mpatanishi nchini humo na kuteuliwa kwa mpatanishi mwingine wakimtuhumu Kodjo, kuegemea upande wa rais Joseph Kabila.
Hatama ya mstakabali wa Congo kuelekea uchaguzi ambao tayari umeahirishwa inaendelea kuleta utata ni kutia hofu ya kutokea kwa machafuko nchini humo, huku jumuiya ya kimataifa ikielezea wasiwasi wao kuhusu machafuko ambayo huenda yakatokea.