Nigeria: kiongozi wa kundi la kigaidi la Ansaru akamatwa
Kiongozi wa kundi la kigaidi la Ansaru nchini Nigeria, lililojitenga kutoka kundi la Boko Haram lenye uhusiano na kundi la AQMI, alikamatwa Ijumaa Aprili 1 katikati mwa Nigeria, jeshi la nchi hiyo limetangaza Jumapili hii.
Imechapishwa:
"Maofisa wa usalama waliendesha operesheni siku ya Ijumaa katika mapambano dhidi ya ugaidi na kumkamata Khalid al-Barnawi, kiongozi wa kundi la kigaidi la Ansaru katika mji wa Lokoja", mji mkuu wa jimbo la Kogi (katikati mwa nchi), msemaji wa jeshi la Nigeria, Rabe Abubakar, amesema.
"Alikuwa kwenye nafasi ya kwanza ya orodha ya magaidi tunaotafuta," Abubakar ameliambia shirika la habari la Ufaransa la AFP.
Wizara ya Ulinzi ya Marekani iliwaorodhesha mwaka 2012 katika orodha ya magaidi wa kimataifa Abubakar Shekau (kiongozi wa Boko Haram), Abubakar Adam Kambar (mwanzilishi wa kundi la Ansaru) na Khalid al-Barnawi.
Al-Barnawi alichukua uongozi wa kundi la Ansaru baada ya kifo cha Kambar wakati wa mashambulizi ya angani ya kijeshi katika maficho yake katika jimbo la Kano, kaskazini mwa Nigeria, Machi 2012.