Burundi: Korti ya Katiba yamruhusu Nkurunziza kuwania muhula wa tatu
Korti ya Katiba nchini Burundi imemruhusu Jumanne wiki hii Rais Pierre Nkurunziza kuwania muhula wa tatu, siku moja baada ya naibu mkuu wa Korti hiyo kuitoroka nchi kutokana na vitisho dhidi yake.
Imechapishwa: Imehaririwa:
Siku moja baada ya maandamano makubwa, ambapo polisi ilitumia risasi za moto na kusababisha vifo vya watu watatu na wengine zaidi ya arobaini kujeruhiwa, kulingana na idadi iliyotolewa na shirika la msalaba mwekundu, maandamano yameendelea leo Jumanne katika wilaya mbalimbali za mji wa Bujumbura.
Korti ya Katiba imemruhusu Rais Nkurunziza kuwania muhula wa tatu katika uchaguzi wa urais unaotazamiwa kufanyika Juni 26, ikibaini kwamba sio kinyume na Katiba ya nchi hiyo. Uamzi huo wa korti umetolewa leo Jumanne asubuhi wakati ambapo naibu mkuu wa Koti ya Katiba, Sylvere Ntimpagaritse aliitoroka nchi Jumatatu wiki hii akileza kuwa Pierre Nkurunziza haruhusiw kuwania muhula wa tatu, bali majaji wamekua wakipata vitisho vya kuuawa iwapo watashindwa kumpitisha rais huyo kuwania muhula huo wa tatu.
Aidha, Makamu wa Rais wa Burundi Prosper Bazombanza ametangaza wakati wa mkutano wa vyama vya siasa uliyoandaliwa chini ya uangalizi wa Umoja wa Mataifa, kwamba serikali iko tayari kuwaachilia huru waandamanaji, kufungua vituo vya redio huria na kuondoa hati za kuwakamata viongozi wa maadamano kwa sharti la kusitisha maandamano.
Katika mitaa mbalimbali ya jiji la Bujumbura, uamzi wa Korti ya Katiba haukuwashangaza wengi. Waandamanaji wanaamini kwamba Korti hiyo ya Katiba iko mikononi mwa utawala wa Pierre Nkurunziza: " Kuna jaji moja tu katika nchi hii, na si mwengine ni Rais Nkurunziza. Lakini sisi hatutositisha maandamano tuliyoanza mpaka pale Pierre Nkurunziza atakapotangaza kuwa hatowania muhula mwengine", waandamanaji wanasema.
Hata hivyo maandamano yameendelea leo Jumanne katika wilaya mbalimbali za jiji la Bujumbura, hata katika mikoa ya Bujumbura, Mwaro na Bururi.