Wanaharakati wa vyama vya kiraia wamuonya Nkurunziza
Wanaharakati wa mashirika ya kiraia nchini Burundi wametishia kutolea wito raia kuingia mitaani iwapo rais Pierre Nkurunziza atatangazwa na chama chake cha Cndd-Fdd kuwania muhula watatu katika uchaguzi wa urais.
Imechapishwa: Imehaririwa:
Chama cha Cndd-Fdd kinatazamiwa kukutana Jumamosi mwishoni mwa juma hili ili kumpitisha rais Nkurunziza kuwania kwa tiketi ya chama hicho katika uchaguzi wa urais uliopangwa kufanyika mwezi Juni mwaka 2015.
Hayo yanajiri wakati vyama vya upinzani vikishirikiana na baadhi ya wafuasi vigogo wa chama tawala cha Cndd-Fdd wametishia tangu Jumatano wiki hii kuingia mitaani ili kupinga nia ya rais Nkurunziza ya kugombea muhula watatu.
Wakati huohuo idadi ya wakimbizi kutoka Burundi inazidi kuongezeka nchini Rwanda. Kambi ya dharura ya Gashora iliyopo wilayani Bugesera kusini mwa Rwanda, tayari imepokea zaidi ya wakimbizi 4800.
Wakimbizi hao wanadai kuwa wamekuwa wakihofia maisha yao baada ya kutishiwa usalam wao na vijana wa Imbonerakure wanaofadhiliwa na chama tawala nchini Burundi cha Cndd-Fdd.
Jumatano wiki hii katika mkutano na waandishi wa habari, Kamisha mkuu wa Umoja wa Mataifa anayehusika na maswala ya Haki za Binadam Zeil Ra'ad Al Hussein akiwa ziarani nchini Burundi alikemea hali ya unyanyasaji wa kisiasa unaotekelezwa na vijana wa chama tawala “Imbonerakure” aliowataja kuwa wanamgambo wa serikali, jambo ambalo limekosolewa na mwenyekiti wa vijana hao Denis Karera.
Denis Karera ameomba Kamishna huyo wa Umoja wa Mataifa kuomba radhi kwa kile alichokiita aliwapaka matope vijana wa chama madarakani “Imbonerakure”.