Morocco: Blaise Compaoré aalikwa na Mfalme Mohammed 6
Aliyekuwa rais wa Burkina Faso, Blaise Compaoré amewasili Morocco akitokea Côte d'Ivoire Alhamisi Novemba 20. Ikulu ya Côte d'Ivoire imeiambia RFI kwamba rais huyo wa zamani wa Burkina faso amejielekeza Morocco kwa mwaliko wa Mfalme wa taifa hilo, Mohammed 6.
Imechapishwa: Imehaririwa:
Blaise Compaoré amekua akiishi katika mji wa Yamoussoukro, baada ya kujiuzulu Oktoba 31 mwaka 2014 kufuatia maandamano ya raia yaliyoitishwa na upinzani pamoja na vyama vya kiraia.
Morocco imejizuia kutoa taarifa yoyote kuhusu sehemu sahihi aliko na muda gani ataishi nchini humo.
Kuondoka kwa Blaise Compaoré nchini Côte d'Ivoire kumezua hisia tofauti katika mji mkuu wa Burkina Faso, Ouagadougou.
Hayo yanajiri wakati bado kunasubiriwa kutangazwa kwa serikali mpya nchini Burkina Faso itakayoundwa na mawaziri 25, huku rais wa mpito Michel Kafando akisubiri kukabidhiwa madaraka ya uongozi wa nchi leo Ijumaa Novemba 21. Marais wa ukanda wa Afrika magharibi wamejielekeza nchini Burkina faso ili kuhudhuria sherehe za kukabidhiwa madaraka rais wa mpito Michel Kafando.
Hata hivyo maandamano yaliyopelekea kuangushwa kwa utawala wa Blaise Compaoré majuma matatu yaliyopita, bado yanaendelea kushuhudiwa katika baadhi ya sekta nchini Burkina Faso.
Wakati ambapo rais Michel Kafando na Waziri mkuu Isaac Zida wakiendelea kujadiliana namna watakavyounda serikali ya mpito, wafanyakazi washirika la umma la utangazaji RTB, wameelezea hasira yao dhidi ya viongozi wa shirika hilo. Wafanyakazi hao ambao walilengwa wakati wa maandamano ya raia majuma matatu yaliyopita, wameomba kufanyike mabadiliko katika shirika la umma la utangazaji RTB.