Ethiopia na Misri zakubaliana kutafuta ufumbuzi juu ya Mgogoro wa Mto Nile
Ethiopia na Misri zimekubaliana kufanya mazungumzo zaidi juu ya athari za Bwawa ambalo limeleta mzozo kati ya nchi hizo, Mawaziri wa Mambo ya nje wa Nchi hizo wameeleza.
Imechapishwa: Imehaririwa:
Waziri wa mambo ya nje wa Ethiopia Tedros Adhanom amesema kuwa wamekubaliana na mwenzake wa Misri,Mohamed Kamel Amr kuanza mazungumzo na kupata maelezo ya kiutaalam na kisiasa.
Nchi hizo ziliingia kwenye malumbano baada ya Ethiopia kuanza kubadili mkondo wa sehemu ya maji ya Mto Nile kwa ajili ya ujenzi wa Bwawa la Nguvu za umeme.
Hata hivyo pamoja na mzozo baina ya nchi hizo, Viongozi hao wamesema kuwa mahusiano yao yataendelea na kuwa watatafutia ufumbuzi Mzozo huo.
Jopo la Wataalam wa kimtaifa lilitoa Ripoti juu ya athari za kupungua kwa kina cha Maji kutaokana na Mradi wa Bwawa hilo, Ripoti ambayo haijawekwa hadharani, lakini Ethiopia imethibitisha kuwa madhara ya kina cha maji ni madogo.
Misri inategemea asilimia 86 ya Maji ya Mto Nile na imesema kuwa ujenzi wa Bwawa ni suala la Kiusalama.