Waasi wa Jamuhuri ya Afrika ya Kati, waridhia kusimamisha mapigano wa kipindi cha Juma moja
Mazungumzo ya kuleta amani kati ya Waasi na Maafisa wa Serikali ya Jamuhuri ya Afrika ya Kati yamepiga hatua muhimu hapo jana baada ya Waasi kusema kuwa wanajiandaa kusitisha mapigano kwa kipindi cha juma moja.
Imechapishwa:
Pande hizo mbili zimekuwa katika mazungumzo tangu siku ya jumatano Mjini Libreville nchini Gabon ambako ni Makao Makuu ya Jumuia ya Kiuchumi ya nchi za Afrika ya kati, ECCAS.
Jumuia hiyo inataka kushughulikia kumaliza Mzozo nchini Jamuhuri ya Afrika ya Kati, ambako Waasi walianza Operesheni zao Tarehe 10 mwezi Desemba na kudhibiti Miji kadhaa nchini humo.
Waasi ambao mpaka jana walikuwa wakishinikiza kuondoka Madarakani kwa Rais Froncois Bozize, pia wanataka Waziri Mkuu mpya achaguliwe kutoka upande wa upinzani.
Bozize aliwasili jana mjini Libreville kuhudhuria Mkutano wa Jumuia ya Kiuchumi ya nchi za Afrika ya Kati ambao pia umehudhuriwa na Rais wa Gabon Ali Bongo, Denis Assou Nguesso wa Jamuhuri ya Congo Brazaville ambaye ni msuluhishi wa Mgogoro na Rais wa Chad Idriss Deby Itno ambaye ni Mshirika wa karibu wa Bozize.