Umoja wa Mataifa wataka wananchi wa Guinea Bissau kuwa watulivu wakati kura zikijumuishwa
Katibu mkuu wa Umoja wa mataifa, Ban Ki Moon amewataka raia wa Guinea Bissau kuwa watulivu baada ya zoezi la kuhesabu kura za urais kuingiliwa kati na mauaji ya aliyekuwa mkuu wa Intelijensia Samba Diallo .
Imechapishwa:
Msemaji wa katibu mkuu huyo, Martin Nesirky amesema Ban amewasifu raia wa nchi hiyo kwa kushiriki zoezi la upigaji kura kwa amani na kuwataka wagombea na wafuasi wote kufuata sheria, kutii matokeo yatakayopatikana na kuepuka vitendo vyovyote vitakavyoharibu utaratibu wa uchaguzi.
Waangalizi wa zoezi la uchaguzi kutoka Jumuia ya kiuchumi ya nchi za Afrika Magharibi, ECOWAS wamesema mbali na kuwepo kwa dosari ndogo ndogo, uchaguzi ulikuwa wa wazi, uhuru na haki.
Mkuu wa ujumbe wa ECOWAS nchini Guinea Bissau, Salou Djibo amesema ujumbe wake una matumaini kuwa uchaguzi huu utafungua milango ya kuelekea kuleta maendeleo ya kisiasa uchumi na usalama.
Kwa sasa zoezi la kujumuisha kura linaendelea na tume ya uchaguzi nchini humo inasema mauji ya Samba Diallo hayatatiza shughuli za tume hiyo.
Kinyanganyiro kikali ni kati ya rais wa zamani Kumba Yala na Spika wa bunge Serifo Nhamadjo.