IATA : Mazingara ni moja ya sababu ya tiketi za ndege kuwa ghali barani Afrika
Usafiri wa ndege barani Afrika una gharama kuliko kusafiri sehemu nyingine duniani. Hayo yameelezwa katika kongamano la siku mbili la wawakilishi wa mashirika ya ndege duniani lililofanyika katika mji mkuu wa Kenya, Nairobi.
Imechapishwa:
Mfano mzuri kuonyesha kuwa usafiri wa ndege Afrika una gharama kubwa ni huu: usafiri wa ndege kutoka mjini Accra, Ghana hadi Nairobi, nchini Kenya unagharimu dola elfu nne za Marikani, na ili hali kusafiri kutoka Accra hadi London, Uingereza ni dola mia tisa sitini.
Adefunke Adeyemi, mkurugenzi mkuu wa chama cha mashirika ya ndege duniani, kinachojulikana kwa kifupi kama IATA, mabye ni mmoja wa waliohudhuria kongamano hilo amesema mojawapo ya sababu ya tiketi za ndege kuwa ghali barani Afrika ni hali ya mazingara. “Mafuta ya ndege ni ghali Afrika. Tiketi za ndege Afrika ni karibu asilimia hamsini kuliko tikiti za ndenge katika sehemu nyingine ulimwenguni”, Adefunke Adeyemiameongeza.
Adeyemi anasema kuwa ushuru wa juu katika viwanja vya ndege Afrika na ushuru unaotozwa kwa mafuta yanayotumiwa na ndege ni asilimia thelathini na tano juu kuliko ushuru ambao unatozwa katika sehemu nyingine ulimwenguni.
Adeyemi amegusia kile ambacho chama cha mashirika ya ndege cha IATA, kinafanya ili kukabiliana na kupunguzwa kwa ushuru katika viwanja vya ndege Afrika.
“Kile ambacho tunafanya kuhusu swala hili la tiketi kuwa ghali Afrika kuliko sehemu nyingine ulimwenguni, ni kuwasiliana na serikali za Afrika mara kwa mara. Nia ya mawasiliano hayo ni kuzifanya serikali za nchi za Afrika kuelewa kuwa kadri gharama ya usafiri wa ndege inapokuwa ndogo, ndivyo watu wengi zaidi watasafiri kwa ndege”, Adefunke Adeyemi amesihi.
Mmoja wa wataalam wa maswala ya usafiri wa ndege nchini Kenya, Mutia Mwandikwa ameelezea kile ambacho nchi za kiafrika zinapaswa kufanya sasa, ikitiliwa maanani kuwa kuna mashirika ya ndege ambayo yamefilisika, kama vile nchini Namibia, Ghana, na Nigeria, na licha ya hayo shirika la ndege la Afrika Kusini, linakabiliwa na matatizo ya kifedha.
“Inafaa nchi zishirikiane zitengeneze shirika ambalo lina nguvu ambalo linaweza kutumikia nchi tofauti ambazo zote zinaweza kupata faida. Kuna kufikiria sana kwa nchi za Afrika kuwa lazima nchi iwe na ndege yake. Afrika tuko na shida ya usimamizi”, Mutia Mwandikwa amesema.
Kongamano hilo lililowaleta pamoja zaidi ya wawakilishi mia moja wa mashirika mbalimbali ya ndege ulimwenguni.