Sintofahamu ya kisiasa yaendelea Maldives
Rais wa Maldives Abdulla Yameen ametangaza hali ya dharula nchini mwake saa chache baada ya kuagiza vyombo vya usalama kuwakamata majaji wa Mahakama ya Juu nchini humo, wakati huu sintofahamu zaidi ya kisiasa ikiendelea kushuhudiwa kwenye taifa hilo.
Imechapishwa:
Kushikiliwa kwa jaji mkuu Abdulla Saeed na jaji mwingine wa mahakama ya juu kumeibusha hali ya wasiwasi na mvutano kati ya mihimili hiyo miwili baada ya rais Yameen kukataa kutekeleza agizo la mahakama lililotaka kuachiwa kwa wafungwa 9 wa kisiasa.
Polisi kwenye visiwa hivyo wamesema kuwa majaji hao wanashikiliwa kwa mahojiano kuhusu tuhuma za rushwa na kwamba maofisa wengine kadhaa wa mahakama ya juu nao wanashikiliwa.
Siku ya Jumatatu Rais Yameen pia aliagiza kukamatwa kwa kaka yake pamoja na rais wa zamani wa nchi hiyo Maumoon Abdul Gayoom ambaye aliunga mkono upinzani.
Yameen mwenyewe ndiye aliyesimamia kukamatwa kwa majaji hao na toka aingie madarakani ameshuhudiwa akiwafunga wanasiasa wengi zaidi wa upinzani.