Maandamano yazuka kufuatia mfumko wa bei Tunisia
Kumekua na maandamano katika mji mkuu wa Tunisia, Tunis, kufuatia mfumko wa bei, maandamano ambayo yamesababisha kifo cha mtu mmoja na wengine watano wamejeruhiwa.
Imechapishwa:
Kwa mujibu wa vyombo vya habari nchini Tunisia, maandamano hayo sasa yameenea katika maeneo mengine nchini humo.
Miongoni mwa sababu ya maandamano hayo ni mfumko wa bei ambao umesababisha kuongezeka kwa kodi katika bidhaa zinaingizwa nchini kama magari na bidhaa nyingine.
Uchumi wa Tunisia umekua ukidorora tangu rais Zine El Abdine Ben Ali alitimuliwa mamlakani mwaka 2011.
Kwa mujibu wa wataalam wa maswala ya uchumi, fedha ya Tunisia imepoteza thamani na sasa imeshuka zaidi ikilinganishwa na Dola au Euro.
Tunisia inategemea misaada kutoka nje kupanda na kuporomoka kwake kwa uchumi.
Kwa mujibu wa wanaharakati wa haki za binadamu nchini Tunisia, polisi wametumia mabomu ya kutoa machozi kuwatawanya waandamanaji wanaopinga kupanda kwa bei za bidhaa mbalimbali.
Wakati huo huo mamia ya watu wameandamana katika mji wa Sidi Bouzid wakipinga juu ya ukosefu wa ajira na maendeleo hafifu katika maeneo yao .